IMEKUWA wiki ngumu
 kisiasa kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambacho  viongozi wake wa 
kitaifa wanahaha kila kona kujaribu kunusuru mgawanyiko  uliopo.
Mambo matatu makuu yanayokiandama chama hicho ni mgogoro wa meya wao na 
 madiwani mjini Bukoba, uchaguzi wa wenyeviti wa halmashauri mkoani  
Kigoma na kukwama kwa propanda zao za ugaidi dhidi ya CHADEMA.
Madiwani wa CCM, CHADEMA na CUF, tayari juzi walimfukuza rasmi Meya wa Manispaa ya Bukoba, Anatory Amani.
Waliopiga kura ya kutokuwa na imani na meya ni madiwani 15 waliosaini  
fomu ya hati ya kumtaka mkurugenzi wa manispaa hiyo kuitisha kikao cha  
dharura kupiga kura ya kutokuwa na imani na meya.
Diwani wa 16 ambaye hakusaini lakini aliridhia uamuzi huo ni Mbunge wa  
Bukoba Mjini, Khamis Kagasheki, ambaye pia ni Waziri wa Maliasili na  
Utalii.
Hata hivyo, haikuwa kazi rahisi kwa madiwani hao kufikia uamuzi huo,  
kwani walikumbana na mikikimikiki ya meya mwenyewe akisaidiana na  
uongozi wa CCM mkoani na Mkuu wa Mkoa wa Kagera, Fabian Massawe.
Habari kutoka vyanzo vya karibu na uongozi wa CCM mkoani Kagera  
vililiambia gazeti hili kuwa kutokana na uamuzi huo, na kwa kuwa CCM na 
 serikali mkoani humo hawataki meya aondoke, chama hicho tawala 
kimepanga  kuwafukuza madiwani wao walioweka sahihi zao kumfukuza meya.
Tayari taarifa zimevuja kwamba CCM itaitisha kikao Agosti 10, mwaka huu 
 kuwafukuza madiwani wake hao ambao wameapa kwamba liwalo na liwe,  
hawawezi kuacha ufisadi utumike kama kigezo cha kuleta miradi Bukoba.
Baadhi ya madiwani waliozungumza na gazeti hili walisema kuwa wanatembea
  na kadi zao za CCM mfukoni tayari kuzikabidhi iwapo uongozi utaamua  
kulinda ufisadi wa meya na kuwachukulia hatua wao.
Vyanzo vyetu vya habari vinasema hatua ya madiwani hao kumwondoa meya  
ilikuwa kama igizo. Mkurugenzi alikataa kuitisha kikao cha baraza la  
madiwani ambacho ndicho kingemfukuza.
Lakini kwa kutambua kuwa idadi iliyohitajika ili meya aondoke ni  
madiwani 16 na tayari ilikidhi matakwa hayo, madiwani hao walikusanyika 
 kufanya uamuzi huo mgumu.
Kabla ya hatua hiyo kufikiwa, juzi asubuhi meya na mkurugenzi wa  
manisapaa hiyo walikwenda mahakamani kuweka pingamizi la kuzuia madiwani
  kuitisha kikao cha kumwondoa meya, kwa hoja kwamba shauri lao lilikuwa
  mahakamani.
Hata hivyo, meya na mkurugenzi waligonga kisiki mahakamani, baada ya  
kuambiwa kuwa shauri lililokuwa mahakamani lilikuwa tofauti na uamuzi  
waliokuwa wanataka kuchukua.
Taarifa hizo zilisema kuwa uamuzi wa meya na mkurugenzi kwenda  
mahakamani ulitokana na agizo la mkuu wa mkoa ambaye alimwandikia  
mkurugenzi huyo akimzuia kuitisha kikao cha baraza la madiwani kama  
alivyokuwa ametakiwa na madiwani hao kwa mujibu wa kanuni.
Baada ya madiwani hao kuona jitihada za meya na mkurugenzi kuzuia azima 
 yao, na walipogundua mahakama imekataa kutoa hati ya zuio la kikao 
chao,  walikusanyika katika ofisi za manispaa hiyo ili kufanya kikao, 
lakini  mkurugenzi alikataa kufungua.
Badala yake waliamua kufanya kikao nje ya ukumbi wa halmashauri,  
wakamfukuza meya na kuandika muhtasari ambao wataupeleka Ofisi ya Waziri
  Mkuu.
Taarifa zaidi zinasema kabla ya hatua hiyo ya madiwani, CCM ilikuwa  
imeitisha kikao cha Halmashauri Kuu ya Mkoa kujadili hatima ya sakata  
hili, hasa madiwani wa chama chao.
Uamuzi wa kuita kikao hicho ulitokana na maagizo ya Makamu Mwenyekiti wa
  CCM Taifa, Phillip Mangula na Katibu Mkuu, Abdulrahman Kinana, ambao  
kwa nyakati tofauti Jumamosi iliyopita waliwasiliana na Mkuu wa Mkoa na 
 Mweyekiti wa CCM Mkoa wa Kagera kuwataka wamalize mgogoro huo “kwa  
busara.”
Katika kikao hicho cha Jumapili, mara baada ya ufunguzi, wajumbe walikaa
  kimya kama walioduwaa. Ndipo alipoibuka mjumbe kutoka Karagwe na kutoa
  hoja kwamba madiwani wa CCM wafukuzwe kwa sababu wanachafua chama.
Hoja yake iliungwa mkono na wajumbekutoka Muleba na Missenyi. Hata  
hivyo, mkuu wa mkoa alionya kwamba hatua ya kufukuza madiwani hao  
ingepingana na ushauri aliopewa na Kinana na Mangula, wa kumaliza  
mgogoro kwa “kutumia busara.”
Akapendekeza kwamba wapewe siku saba za “kujirudi,” waondoe barua yao ya
  kutokuwa na imani na meya; na kwamba baada ya hapo kama watakataa 
ndipo  wafukuzwe.
Inadaiwa kuwa mjumbe mwingine akasema kuwa hata ushauri wa mkuu wa mkoa 
 una dosari, kwa kuwa madiwani hao walikuwa wameshaandika barua kwa  
mujibu wa kanuni, na zilikuwa zimepita siku nne, huku wakihesabu.
Kwa mujibu wa kanuni za halmashauri, barua kama hiyo ikishaandikwa,  
mkurugenzi analazimika kuita kikao ndani ya siku saba baada ya kumpa  
meya taarifa hizo ili ajiandae kujibu tuhuma zinazomkabili.
Mjumbe huyo alimuonya mkuu wa mkoa kwamba halmashauri haiongozwi na amri
  au maelekezo ya mkuu wa mkoa bali kanuni za halmashauri.
Kikao hicho cha Jumapili kiliahirishwa kwa mkanganyiko huo juu ya hatua wanayopaswa kuchukuliwa madiwani hao. 
Hali tete Kigoma
Nako mkoani Kigoma hali ni tete kwa CCM, ambapo Katibu wa Halmashauri  
Kuu (NEC), Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, amelazimika kutua kimya kimya
  kutuliza mgogoro unaofukuta.
Baadhi ya madiwani wa CCM wametishia kuachia ngazi na kujiunga na  
upinzani kwa kile wanachodai kutoridhishwa na uamuzi wa vikao vya uteuzi
  wa wagombea wa uenyekiti wa halmashauri.
Kigoma ni ngome kubwa ya upinzani, ambapo katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 
 2010, kambi hiyo ilizoa viti vitano vya ubunge huku CCM ikiambulia  
vitatu.
Madiwani wanne wa CCM, Elisha Bagwaya (Kibande), Alois Ntilluhoka  
(Biharu), Wilson Ruzibila (Kishanga) na Venance Mporogonyi, wamejaza  
fomu za kuomba nafasi za uenyekiti katika halmashauri mpya ya Buhingwe.
Baada ya madiwani hao kujaza fomu, kikao cha kamati ya siasa ya mkoa  
kilikaa na kurudisha majina mawili ya Bagwaya na Mporogonyi.
Habari za ndani zilidai kuwa madiwani watano kati ya 12 hawakupiga kura 
 kumpata mgombea, ambapo kati ya hao saba waliopiga kura, watano  
walimchagua Bangwanya na wawili walipiga kura za hapana.
Hali hiyo iliibua hofu ya CCM kushinda kiti hicho, hatua iliyolazimu  
chama kuwaita madiwani ambao hawakumuunga mkono mgombea kwenye kamati ya
  maadili ngazi ya mkoa kuhojiwa.
Pamoja na vitisho na ukali kutoka kwa baadhi ya wajumbe, madiwani hao  
walionesha msimamo wao na kusababisha kikao hicho kukosa muafaka.
Mgogoro kama huo umejitokeza katika kikao cha baraza la madiwani  
Halmashauri ya Wilaya ya Kibondo, ambalo lina madiwani wengi wa CCM,  
ingawa mgombea wao alipigiwa kura ya hapana hivyo kufanya mshindi  
kutopatikana.
Halmashauri ya Kibondo ilikuwa inaundwa na halmashauri za Wilaya ya  
Kibondo na Kakonko, ambapo nafasi ya mgombea wa unyekiti alikuwa pekee  
kutoka CCM, Ally Gwanko, aliyepigiwa kura nane za ndiyo na kumi za  
hapana huku makamu mwenyekiti, Emily Mfanye, akipigiwa kura nyingi za  
hapana.
Mkurugenzi wa halmashauri hiyo, Leopard Ulaya, ambaye ndiye msimamizi wa
  uchaguzi huo alisema kuwa kulingana na matokeo hayo kwa mujibu wa  
utaratibu uchaguzi utarudiwa baada ya siku 60.
Hali hiyo imeleta ‘sintofahamu’ ndani ya CCM kutoka na chama hicho kuwa 
 na madiwani 12, ilikinganishwa na sita wa CHADEMA na NCCR-Mageuzi.
Tukio jingine lililoinyong’onyesha CCM wiki hii ni uamuzi wa Mahakama  
Kuu Kanda ya Tabora kulitupilia mbali shitaka la ugaidi lililokuwa  
likiwakabili vijana watano wa CHADEMA.
Uamuzi huo wa mara ya pili baada ya ule wa Mahakama Kuu Kanda ya Dar es 
 Salaam, kufuta mashtaka kama hayo kwa Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama 
wa  CHADEMA, Wilfred Lwakatare, utakuwa pigo kwa CCM kutokana na 
viongozi  wake kutumia propaganda za ugaidi kukichafua CHADEMA.
Naibu Katibu Mkuu wa CCM (Bara), Mwigulu Nchemba na Nape Nnauye  
walitumia tuhuma hizo za ugaidi dhidi ya CHADEMA kuwatisha wananchi wa  
Arusha wakati wa uchaguzi mdogo wa madiwani hivi karibuni.
Mwigulu amekuwa akitamba ndani na nje ya Bunge kuwa anao ushahidi kuwa  
CHADEMA inajihusisha na vitendo vya kigaidi na kwamba angetoa mahakamani
  wakati ukifika.
Kwa uamuzi huo wa Mahakama Kuu ambayo pia imeuonya upande wa Jamhuri  
kuacha michezo ya kugeuza mashtaka ya jinai kuya ya ugaidi, CCM itakuwa 
 imenyong’onyeshwa na propaganda zao hizo.
Source: Tanzania Daima
 
No comments:
Post a Comment