MABINTI WA KIZARAMO NA MAFIGA MATATU-DHANA ILIYOPOTOSHWA NA WAHUNI
  
Inaamini kwa watu wengi kwamba, 
wasichana wa Kizaramo wanapowekwa ndani, hufundishwa kwamba, wakiingia 
kwenye ndoa ni lazima wawe na mafiga matatu.
wanaoamini hivyo wanabainisha kuwa 
mafiga hayo matatu ni ishara ya wanaume watatu, yaani MUME, HAWARA MPYA 
na BWANA WA ZAMANI. lakini pia wapo wanaodai kwamba mafiga hayo matatu 
ina maana ya kuolewa mara tatu katika maisha yake. Hii ikiwa na maana 
kwamba, mwanamke wa kizaramo ni lazima aolewe na kuachwa mara tatu 
maishani mwake.
Tafsiri hiyo ni uhuni tu wa watu 
wachache wanaotaka kupotosha watu, lakini hakuna ukweli wowote kuhusiana
 na madai hayo. Ni kweli kwamba wasichana wanawali wa Kizaramo 
hufundishwa kuhusu mafiga matatu pale wanapokuwa wamewekwa ndani kwa 
ajili ya kufundwa kwa mujibu wa mila na desturi za kizaramo. Lakini 
mafiga hayo matatu huwakilisha watu tofauti na sio mume, hawara mpya 
wala bwana wa zamani, ni uzushi tu na uhuni wa watu wachache wanaopenda 
kudhalilisha mila za wenzao.
Mafiga matatu yanaozungumziwa, 
huwakilisha, watu muhimu kwenye maisha ya ndoa ya mwanamke yeyote. Figa 
la kwanza ni MUME, figa la pili ni NDUGU WA MUME, yaani mawifi na 
mashemeji zake, figa la tatu ni WAZAZI WA MUME, yaani wakwe.
Msichana wa kizaramo anapokuwa katika 
kufundwa, huelekezwa namna anavyotakiwa kuishi na watu hao, yaani mafiga
 hayo matatu. Anafundishwa namna ya kumtendea mume wake katika mazingira
 tofauti, hufundishwa namna ya kuishi vizuri na wakwe zake, na namna 
anavyoweza kuwakabili mawifi na mashemeji zake kwenye mazingira yote.
Ni kawaida ya Wazaramo kuwafundisha 
watoto wao wa kike namna ya kuweza kuishi na ndugu za watakaokuwa waume 
zao. Msichana wa Kizaramo anatakiwa kufahamu namna ya kutumia mafiga 
hayo bila figa lolote kuondoka, kwa sababu kama litaondoka figa moja, 
hataweza kubandika chungu katika mafiga yaliyobaki. Hii ina maana 
kwamba, bila kuwa na uelewano na na wote hao watatu, ndoa yake inaweza 
kuwa katika matatizo.
Ukweli ni kwamba, wasichana wa Kizaramo 
ambao wamezingatia kweli kile walichofundishwa, wakati wanafundwa, 
hutokea kuwa wanawake waadilifu sana, kuliko inavyodhaniwa. kuna 
ushahidi wa kutosha kwa wanawake wengi wa kizaramo ambao wameolewa huko 
Bara, ambao wamewashangaza wengi kwa nidhamu yao ya hali ya juu.
Source:Jamii Forums
 
 
 
          
      
 
  
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment