NA: Charles Misango 
ALIJULIKANA shule nzima kama sio kata kwa kutandika wanafunzi 
bakora. Alikuwa ni mwalimu aliyeogopwa na kila mwanafunzi, sio kwa 
sababu ya bakora zake, bali kwa mtindo aliochagua kukuadhibia.
  Kwanza ni tabia yake ya kuchapa bakora kwenye makalio ya mwanafunzi 
akiwa amesimama, bila kujali kama ni mvulana au msichana. Lakini kubwa 
zaidi, alichukia sana kusikia sauti ya kilio au kwikwi ya mwanafunzi 
aliyekuwa akilambwa bakora.
  Mwalimu huyu ili akusamehe au apunguze idadi ya bakora alizopanga 
kukutandika, ulilazimika ama unyamaze au ugugumie kila mkono wake 
uliposhuka makalioni.
  Lakini zaidi alifurahi kusikia mwanafunzi akicheka na kusema ‘asante 
mwalimu’ kila fimbo ilipomwingia barabara; kwamba mwalimu huyo 
angejisikia furaha kubwa, kama baada ya kumaliza adhabu hiyo kumwambia, 
“Nakushukuru mwalimu Makomba kwa zawadi tamu.”
  Ilikuwa ni kumpandisha hasira ikiwa mwanafunzi aliondoka kimya kimya 
au akianza kulia baada ya kutandikwa.  Eti ilikuwa sawa na kudharau 
adhabu yake! Ilionesha adhabu ile ilikuwa ya uonevu na kilio cha 
mwanafunzi kilikuwa ishara kwake kuwa ipo siku naye atalipiza!
  Nimelazimika kukumbuka vituko vya mwalimu huyu (sasa ni marehemu) 
kutokana na ambacho wakulima wa Tanzania wamelazimishwa kwa miaka kadhaa
 sasa kufanana na tuliokuwa wanafunzi chini ya mwalimu Makomba.
  Serikali ama kwa nia njema au kwa kuzuga tu, kwa miaka mingi sasa 
imekuwa ikiendeleza utaratibu wa siku nyingi wa kile wanachokiita 
sherehe wakulima ya Nanenane.
  Nakiri kwamba ingawa nilikuwa bado mdogo, lakini nakumbuka mwanzoni 
mwa miaka ya sabini, sikukuu ya wakulima ilikuwa kubwa na yenye fahari 
kwa wakulima.
  Ilikuwa inasuburiwa kwa hamu kubwa na wakulima wengi lakini zaidi wale
 wa pamba na mazao mengine ya biashara kwa sababu wakati huo ikifanyika 
baada ya mauzo ya pamba.
  Hata wale wa mazao ya chakula waliipokea kwa furaha kubwa kwa sababu 
nao kwa wakati huo walikuwa wameuza mazao yao na kwa kweli walikuwa 
‘wamefurika mapesa’.
  Nakumbuka hotuba za wakulima hazikutolewa na wanasiasa, bali wao 
wenyewe. Kila kijiji kilikuwa na risala yake iliyojaa maelezo ya ukweli 
ya kipi wanakihitaji na kipi wanashukuru kwa kupewa na serikali kutokana
 na mahitaji waliyoomba wakati wa sherehe za mwaka uliotangulia.
  Ni sherehe zilizoambatana na maonesha ya mazao bora na mshindi kwa 
kila kijiji alipewa zawadi ya zana za kilimo. Nakumbuka mkulima mmoja 
katika kijiji cha Sanza, wilaya ya Manyoni, mkoani Singida aliyepewa 
zawadi ya trekta na Mwalimu Nyerere baada ya kuwa mkulima bora wa 
wilaya. Sijasahau namna mzee huyo alivyoruka juu kwa furaha huku akitoa 
machozi.
  Nakumbuka bado wakulima wengine waliozawadiwa majembe ya kukokotwa na 
ng’ombe ngazi za vijiji, mbolea na baadhi kupelekwa kusomeshwa katika 
vyuo vya kilimo vya ndani ya nchi. Sijasahau namna wakulima 
walivyoshindana na wafugaji katika michezo ya mpira wa miguu, bao, ngoma
 na mambo mengine mengi.
  Ni sikukuu ambayo enzi hizo ilileta maana kamili ya sherehe ya wakulima.
  Pamoja na kwamba kilimo kilitegemea jembe la mkono, wazazi wetu 
waliipenda  kwa sababu walithaminiwa, walitendewa haki na walijua 
wanalima wakiwa na uhakika wa soko na bei.
  Leo yametoweka haya yote. yamebaki masimulizi. Hakuna mkulima wa kweli wa kijiji anayeonja tena ladha na tamu ya Nanenane.
  Sherehe hizi zimetekwa na wanasiasa na wachuuzi wa mazao.
  Zimebaki kuwa miradi ya waroho na wenye uchu wa fedha za wanyonge, kupata mwanya wa kutafuna fedha za kodi ya wanyonge.
  Tofauti na zamani ambapo watawala walionyesha kwa matendo thamani ya 
mkulima, leo imebaki kama enzi ya mwalimu Makomba; kwamba mkulima wa 
korosho ambaye mwaka mzima alilazimishwa kununua pembejeo kwa bei ya 
kulangua iliyopangwa na makuwadi wa soko  na kubarikiwa na watawala, 
analazimishwa ashangilie kwa maandamano na nyimbo sikukuu ya Nanenane.
  Mkulima yule yule ambaye amenyimwa uhuru wa yeye kupanga bei ya mazao 
yake kulingana na gharama na nguvu kazi alizotumia katika uzalishaji, 
lakini sasa analazimishwa kuuza kwa bei ndogo ambayo haiwezi kurudisha 
hata bei ya pembejeo, analazimishwa kwenda uwanjani kulikopambwa mapambo
 yaliyogharimu mamilioni ya fedha na kutwangwa jua, ili kusikiliza 
hotuba za watawala.
  Bila kujali unyonge na jasho lake, mkulima huyu ambaye pamoja na 
kufanyiwa yote hayo, amenyimwa malipo ya pili baada ya kuuza kwa mtindo 
wa stakabadhi gharani, kwa sababu eti mazao yake yameshuka bei katika 
soko la dunia, anaambiwa aje kwenye sikukuu yake, kushuhudia namna  ya 
mashindano ya magari ya kifahari yaliyojipanga viwanjani na maelfu ya 
maafisa wa serikali wanaolipwa posho za malaki.
  Wanataka mkulima huyu ambaye ameshindwa kupeleka watoto wake shule kwa
 kukosa ada kutokana na jua na viwavijeshi kuangamiza mazao yake  bila 
msaada wa serikali ashangilie na kuipongeza serikali. Kwamba badala ya 
kulia na kusaga meno kwa kule kutojua kwake ataishi vipi kwa mwaka 
mzima, wanataka acheke, aruke, acheze!
  Watawala wanamwambia mkulima aliyenyang’anywa shamba lake ambalo 
amelimiliki miaka na miaka bila fidia, kisa eti kapewa mwekezaji, kama 
alivyotufanyia mwalimu Makomba, analazimishwa ashangilie eti ni sikukuu 
yake!
  Kama Mwalimu Makomba  alivyotufanyia, watawala wetu walioshuhudia  
mkulima akipigwa, kuswekwa ndani na kufunguliwa mashitaka ya uchochezi 
kwa kule tu kupinga kwake kuporwa ardhi yake kwa fidia kiduchu wanataka 
naye ashangilie na kuifurahia sikukuu ya nanenane.
  Watawala wanataka mkulima wa Ukara kwetu kule, Msimbati, Kifulwe, 
Nkojingwa na kwingine ambako mara ya mwisho kumwona kiongozi wa juu 
ilikuwa miaka kumi iliyopita baada ya kutembelewa na mkuu wa wilaya; 
kule ambako hawajui kama kuna suala la maji ya bomba, eti naye amshukuru
 Mungu kwa kupewa siku ya kupumzika na kufurahia matunda ya kilimo 
chake!
  Nani anayemjali mkulima huyu hata amfanyie sherehe? Mkulima gani 
katika sherehe anashangilia ikiwa, maisha yake yametoswa na haonekani 
kuwa wa maana? Ni mkulima gani mwenye akili timamu anayeweza kuthubutu 
kushangilia nanenane huku, watoto wake wakiwa wametawanyika mijini 
wakiuza soksi za mitumba baada ya ng’ombe wa wafugaji  wenye sauti na 
nguvu za fedha kulisha mazao yake yote nay eye kuponea chupuchupu kuuawa
 akijaribu kujitetea?
  Ni mkulima gani makini anayeweza kufurahia nanenane ikiwa, binti zake 
wamelazimika kuolewa baada ya kukosa ada ya kuwasomesha kwa sababu, 
alilazimishwa kununua mbolea feki iliyoangamiza sio tu mazao bali na 
kuharibu ardhi yake?
  Nani na wa wapi mkulima yule atakayesikiliza hotuba na ngoma za 
wanasiasa ambao wameishia kutoa matamshi ya kulaani mawakala wa 
kishetani waliomuuzia mbolea lakini wasikamatwe na kushitakiwa ikiwa ni 
pamoja na kulipwa fidia?
  Hivi katika taabu na maumivu yote haya, yakiwemo ya mkulima kukosa 
usafiri wa uhakika wa mazao yake, wizi wa walanguzi wa lumbesa, kupigwa 
marufuku na kunyimwa uhuru wake wa kuuza mahindi, mtama, korosho, mchele
 na mengine popote anapoona kuna maslahi, mnataka awe kama Mwalimu 
Makomba alivyotuamuru kucheka na kumwambia ‘asante Mwalimu kwa bakora 
tamu?’
Chanzo:TanzaniaDaima 
 
No comments:
Post a Comment