NCHEMBA ATUHUMIWA KUSHUSHA HESHIMA YA CCM
 
MATUKIO kadhaa ya kisiasa, mwelekeo, 
kauli na mienendo ya baadhi ya wanasiasa waandamizi na wenye nguvu 
katika Chama cha Mapinduzi (CCM) vimeibua mkanganyiko na hali tete ndani
 ya chama hicho, Tanzania Daima Jumamosi limebaini.
Kwa muda sasa, kumekuwa na minyukano ya 
ndani kwa ndani miongoni mwa viongozi waandamizi wa CCM, huku baadhi yao
 wakilaumiana kwa “kuchafua na kuua” chama.
Baadhi yao wamefikia hatua ya kumlaumu 
Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete, kwa kuwapa madaraka makubwa 
baadhi yao, na kushindwa kuwanyang’anya pale wanapoonyesha dalili za 
“kuua” chama chao.
Gazeto hili linazo taarifa za baadhi ya 
viongozi wastaafu wa CCM kupeleka ujumbe mzito kwa Makamu Mwenyekiti, 
Phillip Mangula, wakionyesha kukerwa na kauli au mwenendo wa baadhi ya 
viongozi waandamizi, hasa Naibu Katibu Mkuu, Mwigulu Nchemba.
Wanamtuhumu Nchemba kwa kushusha heshima
 ya CCM mbele ya umma, na kuchangia matokeo mabaya katika uchaguzi wa 
madiwani uliofanyika Arusha mwezi uliopita, ambako CCM ilishindwa na 
CHADEMA katika kata zote nne.
Baadhi ya wazee na makada waandamizi 
wanasema Nchemba ni “mzigo wa Kikwete,” kwa maana kuwa ndiye aliyempa 
madaraka, na ndiye anayemsikiliza na kumpa jeuri.
Nafasi anayopewa Nchemba imeleta 
mgongano wa chini kwa chini kati yake na Katibu wa itikadi na Uenezi, 
Nape Nnauye, ambaye kwa muda sasa amekuwa ndiye kipenzi cha Rais Kikwete
 katika kutekeleza mikakati kadhaa na kutoa matamko yenye utata dhidi ya
 viongozi au wanachama “wasiopendwa” ndani ya chama hicho, au dhidi ya 
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
Kwa mujibu wa makada wanaokerwa na tabia
 ya Nchemba, kiongozi huyo amegeuka kero kwa viongozi wenzake, ambao 
wanasema ameingiza siasa za ujasusi wa waziwazi na mbinu nyingine chafu 
za kisiasa zinazomfanya aibomoe CCM na kuiongezea umaarufu CHADEMA mbele
 ya umma.
Source:Tanzania Daima
 
 
 
          
      
 
  
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment