
Serikali ya Rwanda imetoa tamko linaloonyesha kutoielewa kauli ya Rais Jakaya Kikwete, iliyoamuru wahamiaji haramu kuondoka nchini, hali inayoonekana kukwepesha hoja.
Rwanda kupitia waziri wake wa Mambo ya Nje, Louise
 Mushikiwabo, ilikaririwa ikieleza kwamba hawatajibu mapigo agizo la 
Rais Jakaya Kikwete ya kuwataka Wanyarwanda wote waliolowea Magharibi 
mwa Tanzania kuondoka haraka.
                
              
Mushikiwabo alisema wako tayari kuwapokea na 
kuwalinda wote waliofukuzwa Tanzania kwa kisingizio kuwa ni wahamiaji 
haramu, akieleza kwamba anasikitishwa kwa kuwa Tanzania haikufanya 
jitihada yoyote kuwasiliana na Rwanda kuhusu suala hilo kabla ya 
kuchukua uamuzi huo.
  
                
              
“Ni uamuzi ambao umeshachukuliwa, 
hatukushirikishwa kwa namna yoyote na jukumu letu kama serikali na taifa
 ni kuwahakikishia ulinzi wote wanaokuja, na hili ndilo suala 
tunalolishughulikia kwa sasa,” alisema.
                
              
Kwa mujibu wa gazeti la New Times, Mushikiwabo 
aliwaeleza waandishi wa habari kwamba agizo hilo la Rais Kikwete pamoja 
na ushauri wa kuitaka Serikali ya Rwanda kuzungumza na wanamgambo hasimu
 wa FDLR waliopo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), hayatayumbisha 
uhusiano imara baina ya Watanzania na Wanyarwanda.
  
                
              
“Sisi si majirani tu, tuna mfungamano imara baina 
ya watu wetu pia, tuna mfungamano wa damu, wa kibiashara, na mengine 
mengi ya kutufanya tuendelee kuwa pamoja,” alisema na kutumia fursa hiyo
 kuwakaribisha Watanzania nchini Rwanda.
 
                
              
Watanzania wanaweza kuishi hapa kwa umri wowote 
wanaotaka. Tunawachukulia kuwa ni watu wetu muhimu kwenye fungamano la 
Jumuiya ya Afrika Mashariki,” alisisitiza.
                
              
Rais Kikwete wakati akihitimisha ziara yake mkoani
 Kagera alitoa agizo la kuwataka wanaomiliki silaha kinyume cha sheria 
na wahamiaji haramu ama kuondoka au kuhalalisha ukazi wao, huku akitoa 
wiki mbili kwa zoezi hilo kutekelezwa, kabla ya kuanza kwa operesheni ya
 kuwasaka watu hao.
                
              
Kauli hiyo ilitokana na kushamiri vitendo vya 
kihalifu katika eneo la Kanda ya Ziwa, Rais hakutaja jina la nchi ya 
wahamiaji hao. Kwa ukanda huo Tanzania inapakana na Kenya, Uganda, 
Rwanda, Burundi na DRC.
                
              
Pia, Rais Kikwete katika hotuba yake ya mwisho wa 
mwezi alizungumzia kusikitishwa na kauli za shutuma, kejeli na 
udhalilishaji zilizotolewa na Rais Paul Kagame wa Rwanda dhidi yake.
                
              
Mvutano baina ya Rwanda na Tanzania ulianza 
kuwekwa hadharani Mei mwaka huu, baada ya Rais Kikwete kuishauri Rwanda 
kukaa na kuzungumza na FDLR wenye makao yao DRC, hatua ambayo 
haikuifurahisha Serikali ya Rwanda.
                
              Wakati Rwanda ikieleza hayo jana Katibu Mkuu Kiongozi, Ombeni Sefue alizungumza na gazeti hili, na kutaka majibu ya kauli hiyo ya Rwanda yatolewe na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje, Mkumbwa Ally alisema kauli 
iliyotolewa na Rais Kikwete ilikuwa ni ushauri, kwamba Rwanda wanaweza 
kuukubali ama la.
“Kilichomkasirisha Rais Kikwete ni lugha za matusi
 zilizokuwa zikitolewa na viongozi wa Rwanda, ila kwa hicho 
walichokisema sidhani kama kitakuwa na tatizo kwetu,” alisema Mkumbwa.
  
Alifafanua kwamba, alipokuwa mkoani Kagera Rais 
Kikwete hakutoa agizo la Wanyarwanda kufukuzwa, bali alitoa agizo la 
kuanza kwa operesheni ya kuwakamata wahamiaji haramu, wale wanaomiliki 
silaha kinyume na taratibu.
“Rais alizungumzia masuala ya jinai ‘Criminal Element’, siyo kuwafukuza Wanyarwanda,” alisisitiza.
Hatutazungumza na FDLR
Waziri wa Mambo ya Nje, Louise Mushikiwabo, 
aliendelea kusema sera ya Rwanda kuhusiana na makundi ya aina hiyo, iko 
wazi na haitabadilika, kauli ambayo amekuwa akiirudia kila mara na 
kuwataka wote wanaofikiria kuhusu Rwanda kuzungumza na FDLR kwa namna 
yoyote kusahau wazo hilo.
“Kama umehusika kwa namna yoyote na maangamizi, 
wewe utakuwa adui wa kila mtu. Ni wazi kwamba Wanyarwanda wote watakuwa 
kwenye majonzi iwapo kwa namna yoyote kutakuwa na mawasiliano ya FDLR,” 
alifafanua.
Kundi la FDLR ambalo ni kifupisho cha Democratic 
Forces for the Liberation of Rwanda, linaundwa na watu walioshiriki 
kwenye mauaji ya kimbari yaliyowalenga watu wa kabila la Watutsi mwaka 
1994, na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 800,000 kwa miezi mitatu.
Kundi hilo ambalo limeweka makazi yake mashariki 
mwa DRC, linadaiwa kufanya mashambulizi kadhaa yakiwamo ya milipuko ya 
mabomu nchini Rwanda, ambapo mwezi uliopita shambulio la aina hiyo mjini
 Kigali lilisababisha vifo vya watu watatu na kujeruhi watu kadhaa.
Uhusiano wa kihistoria
Familia za Rwanda zikiwamo zilizoishi Tanzania 
tangu miaka ya 1950, zimeelezwa kuwa zimekuwa zikiwasili nchini humo 
kupitia mpaka wa Rusumo baada ya agizo la Rais Kikwete kuwataka wawe 
wameondoka ndani ya wiki mbili, kabla ya kuanza kwa operesheni rasmi ya 
kuwaondoa.
  
Kwa mujibu wa mamlaka nchini Rwanda, mamia ya 
Wanyarwanda waliokuwa wakiishi mkoani Kagera ambako ndiko Tanzania 
inapopakana na Rwanda wamekuwa wakirejea kwa wingi, ambapo hadi juzi, 
zaidi ya watu 300 walikuwa wameshaorodheshwa kwenye ofisi za Uhamiaji.-Mwananch
 
No comments:
Post a Comment