Hali tete CCM Bukoba,Madiwani wamgeuka Kikwete, wafanya kinyume na maamuzi yake
.Hongo yatembezwa, madiwani watishwa kung’olewa
HATUA ya madiwani wanane wa Chama cha Mapinduzi (CCM) katika manispaa ya
 Bukoba, kusaini hati ya tuhuma na kuiwasilisha barua hiyo kwa 
mkurugenzi wa manispaa hiyo, kumtaka aitishe kikao ili wapige kura ya 
kutokuwa na imani na meya anayetuhumiwa kujiingiza katika miradi ya 
kifisadi imechukua sura mpya.
  Taarifa zilizolifikia gazeti hili 
jana jioni kutoka mjini Bukoba, zilisema kuwa msimamo huo umewagawa 
viongozi wa CCM mkoa wa Kagara na hivyo kuitisha kikao cha halmashauri 
ya mkoa leo kwa ajili ya kuwajadili na kuwafukuza madiwani hao.  Hata
 hivyo uamuzi huo, huenda ukakigharimu chama hicho kutokana na madiwani 
hao kusisitiza msimamo wao, wakisema wako tayari kufukuzwa kwa sababu 
wanatetea maslahi ya wananchi wakipinga ufisadi.
  Akizungumza kwa simu na gazeti 
hili kwa masharti ya kuhifadhiwa jina lake, mmoja wa madiwani hao 
alisema kuwa rushwa imekuwa ikitembezwa waziwazi kwa wajumbe wa vikao 
mbalimbali vya CCM ili kuwalazimisha wakutane mara kwa mara kufikia 
uamuzi huo.  Chanzo hicho 
kimedokeza kuwa katika kuwagawa madiwani hao ambao wameungana na wenzao 
wa vyama vya CHADEMA na CCM ili kupunguza idadi ya akidi, diwani mmoja 
alijaribiwa kuhongwa milioni 20 ili aondoe jina lake katika orodha hiyo.
  “Mwenzetu mmoja kwa kweli amekuwa 
jasiri wa ajabu, juzi aliitwa mahala akatumiwa watu wakiwa na fedha 
taslimu milioni 20 lakini alikwepa mtego huo na kuwakimbia watu 
waliotumwa, akisisitiza kuwa hawezi kutusaliti. Sasa kwa hali hii kama 
CCM wanadhani wanaweza kukinusuru chama kwa kutufukuza na wajaribu 
waone,” alisema.  Naye diwani
 mwingine alidokeza kuwa baadhi ya viongozi wa CCM wilaya na mkoa ndio 
wanatumika kuwarubuni madiwani hao kwa rushwa ili waondoe tuhuma hizo 
dhidi ya meya, Anatory Amani.
  Hivi karibuni, madiwani hao 
walimgeuka Rais Jakaya Kikwete, wakipinga uamuzi wake wa kumtaka meya 
kumaliza tofauti zake na mbunge wa Bukoba mjini, Balozi Khamis Kagasheki
 kwa kile walichodai mgogoro huo si ugomvi kati ya wawili hao.  Madiwani hao walipinga kauli hiyo wakisema suluhu ni kupinga ufisadi wa meya, kwani hakuna ugomvi binafsi kati yake na mbunge.
  Akihutubia mkutano mjini Bukoba, 
Rais Kikwete alisema ujenzi wa soko kuu la kisasa katika manispaa hiyo 
lazima uendelee na kwamba hakuna hoja ya kuendelea na malumbano 
“yasiyokuwa na msingi”.
  Madiwani hao 15 walisema malumbano
 yaliyopo ni ya msingi kwa kuwa watu watakaobebeshwa deni la kurejesha 
mikopo inayochukuliwa na meya ni wakazi wa Bukoba, si meya mwenyewe.  Walisema
 Rais ameonekana hafahamu kiini cha mgogoro, kwani kinachopingwa si 
miradi, bali utaratibu ambao meya ametumia kuanzisha miradi hiyo 
kifisadi bila kuzingatia maslahi ya wananchi.
  Miradi hiyo ni upimaji wa viwanja 
5,000 unaodaiwa mkopo wake wa sh bilioni 2.9 kutoka Mfuko wa Dhama ya 
Uwekezaji (UTT) haukufuata taratibu, na wananchi hawakushirikishwa 
ipasavyo.  Tuhuma nyingine ni
 mradi wa ujenzi wa soko. Meya anadaiwa kusitisha malipo ya ushuru na 
kutaka kuwaondoa wafanyabiashara bila kufuata utaratibu.
  Anatuhumiwa pia kukopa sh milioni 
200 kutoka Benki ya Uwekezaji (TIB) bila kibali cha Baraza la Madiwani. 
Vile vile alitoa taarifa kwenye kikao cha baraza hilo kuwa TIB iliwapa 
ruzuku ya sh milioni 90, lakini hakueleza misingi yake.
  Upo pia mradi wa kuosha magari 
ambao unadaiwa kutumia kiasi cha sh milioni 297 zinazotiliwa shaka. 
Ameshindwa pia kutoa mchanganuo wa mapato na matumizi ya mradi ya kiasi 
cha sh milioni 134, za ujenzi wa kituo cha mabasi.
  Barua ya madiwani hao, 
iliwasilishwa jana asubuhi saa 2.30 na kupokelewa na Mkurugenzi wa 
Manispaa hiyo, Shimwela L.E, ikiwa na saini za madiwani 16 kati ya 24 
waliopo.  Hata hivyo, 
mkurugenzi huyo, alipotafutwa na gazeti hili alishindwa kukiri au 
kukanusha kupokea barua hiyo, akisingizia kuwa kwa muda huo alikuwa 
akitekeleza majukumu yake nje ya ofisi.  “Unajua
 Rais juzi aliacha maagizo mengi na baya zaidi ni lile la ugawaji wa 
viwanja, hivyo asubuhi niliingia ofisini na kutoka kuelekea mitaani. 
Nitakupa taarifa kesho kama barua hiyo imefika,” alisema.
  Kwa mujibu wa kanuni za manispaa 
hiyo yenye madiwani 24, watatu wa CUF, wanne wa CHADEMA na 17 wa CCM, 
ili kupitisha uamuzi huo wa kumuondoa meya, ni lazima robo tatu ya 
madiwani yaani 16, wapige kura ya kuunga mkono hoja hiyo.
  Kanuni hizo pia zinaelekeza kuwa 
mkugenzi atapaswa kuitisha kikao hicho ndani ya siku saba kuanzia tarehe
 aliyopokea barua ya tuhuma hizo za madiwani na ndani ya muda huo 
anapaswa kuwa amempatia mtuhumiwa tuhuma hizo ili aweze kuzijibu.
  Alisema walikuwa wamesaini 
madiwani 16 lakini waliamua kumtoa Balozi Kagasheki kwa vile ni waziri 
na sehemu ya serikali, hivyo walibakia madiwani 15. Hata hivyo, 
inajulikana kuwa hata Kagasheki anawaunga mkono itakapofika hatua ya 
kupiga kura ya kutokuwa na imani na meya.  Madiwan
 hao wanaompinga meya ni Richard Gaspar (CCM), Rabia Badru (CUF), 
Murungi Kichwabuta (CCM), Winfrida Mukono (CHADEMA), Alexander Ngalinda 
ambaye pia ni Naibu Meya (CCM), Yusuf Ngaiza ambaye pia ni Mwenyekiti wa
 CCM wa wilaya, Deusdedit Mutakyahwa (CCM), Robert Katunzi (CCM), Samwel
 Ruhangisa (CCM) na Dauda Kalumuna (CCM).
  Wengine ni Dismas Rutagwelela, Israel Mlaki wa CHADEMA na Conchester 
Rwamlaza ambaye pia ni mbunge wa Viti Maalum wa chama hicho pamoja na 
Ibrahim Mabruk, Felician Bigambo wa CUF.
Sosi : Tanzania Daima
 
 
 
          
      
 
  
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment