 
 
Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh 
Ponda Issa Ponda amesema alichanganyikiwa kiasi cha kushindwa kujielewa 
kwa muda baada ya kupigwa risasi.
  
Akizungumza 
katika mahojiano maalumu na Mwananchi kwenye wodi binafsi ya Taasisi ya 
Tiba ya Mifupa Muhimbili (Moi) alikolazwa jana, Sheikh Ponda alisema 
kutokana na hali hiyo hakumbuki matukio yaliyofuata baada ya hapo.
  
 
“Sikumbuki
 hata nilipata huduma ya kwanza hospitali gani kwa sababu sikuwa katika 
hali ya kawaida. Mambo mengine yaliyotendeka kabla ya kujeruhiwa 
ninayakumbuka vizuri,” alisema Ponda ambaye inasadikiwa kwamba alipigwa 
risasi ya begani, Ijumaa iliyopita mjini Morogoro.
  
 
Alisema
 alihutubia katika Kongamano la Waislamu kwa muda mfupi akizingatia muda
 uliokuwa umetolewa kumaliza mkutano huo na baada ya hapo alishuka na 
kupanda kwenye gari binafsi ambalo lilizingirwa na polisi ndipo akaamua 
kushuka na kuanza kutembea kabla ya kujeruhiwa.
  
 
Mahojiano maalumu na Sheikh Ponda
 
Swali: Je, watu waliokupa huduma ya kwanza mara baada ya kujeruhiwa walikuta risasi iliyokujeruhi?
 
Jibu:
 Nilipigwa risasi kwa nyuma ikatokea mbele kwa hiyo haikubaki mwilini 
wala haikuonekana ilipoangukia kwa wakati huo maana kulikuwa na 
purukushani.
 
Swali: Ulipata wapi huduma ya kwanza?
 
Jibu:
 Kwa kweli kwa sasa siwezi kukumbuka nilihudumiwa wapi kwa sababu mara 
baada ya kujeruhiwa sikuwa katika hali yangu ya kawaida, 
nilichanganyikiwa.
 
Swali: Utathibitisha vipi kama ulipigwa risasi?
 
Jibu:
 Bahati nzuri ni kwamba tukio hili lilitokea kweupe wapo wengi 
walioshuhudia, kwa hiyo wanaweza kusaidia kuthibitisha na ushahidi 
mwingine ni jeraha hili.
  
 
Swali: Nini msimamo wako baada ya tukio?
Jibu:
 Nitaendelea kuzungumzia haki za Waislamu na siwezi kurudi nyuma. Pamoja
 na kwamba wananiona mimi ni mtu mchochezi lakini wanaeneza chuki dhidi 
yangu kwa njia wanazojua wao. Nitaendelea, risasi haitaninyamazisha.
  
 
Swali: Umehusishwa kufanya uchochezi Zanzibar, unalizungumzia vipi hilo
 
Jibu:
 Zanzibar nilichozungumza ni kuhusu kesi dhidi ya viongozi wa Kundi la 
Uamsho. Watu wamewekwa ndani kwa miezi tisa sasa, kwa mujibu wa sheria 
za nchi yetu, kesi wanayoshtakiwa ina dhamana, sasa nikauliza kwa hao 
viongozi, kwa nini hawazingatii sheria?
  
 Kesi zina muda mrefu hazitolewi 
uamuzi, nikawasisitiza wazingatie misingi ya sheria kwa kuwa hivyo 
wanavyowatendea wananchi wajue kwamba hawastahili kupewa tena ridhaa ya 
kuongoza nchi, nilifikisha ujumbe wangu.
 
Swali: 
Kuna tukio la kumwagiwa tindikali mabinti wawili wa Uingereza 
lililotokea Zanzibar, ambalo wewe pia unahusishwa, hili 
unalizungumziaje?
  
 
Jibu: Sijaona huo ushahidi ambao 
wanahangaika kunihusisha na tukio hilo, nahusishwa vipi? Matukio ya 
kumwagiwa tindikali yamekuwa yakijitokeza mara kwa mara huko kabla 
sijakwenda kuhutubia. Vyombo vya dola vifanye kazi yake vyema ili 
kubaini ukweli wa jambo hili.
  
 
Pia Mwananchi ilizungumza na mke wake, Sheikh Ponda, Hadija Ahmad ambaye alikuwa ameketi pembeni ya kitanda alicholazwa mumewe.
  
 
Swali: Unazungumziaje tukio hili la kujeruhiwa kwa mumeo?
 
Jibu:
 Hili ni dhumuni la Serikali, lililenga moja kwa moja kumdhuru ili 
kunyamazisha harakati zake za kutetea wanyonge. Ni tukio la kupangwa, 
halijatokea bahati mbaya. Serikali inamfuatilia sana hivyo ililenga 
kumnyamazisha.
  
 
Namshauri Rais (Jakaya Kikwete), 
kuhakikisha kwamba haki za wanyonge zinawafikia, asije akafikiri hili 
lililotokea kwa Sheikh Ponda ni suluhisho, ni vyema kufanya mazungumzo 
ili kuweka mabadiliko.
 
Mtu
 wa karibu wa Sheikh Ponda alisimulia jinsi walivyomsafisha kiongozi 
huyo kutoka Morogoro hadi Dar es Salaam na kukwepa vizuizi vya polisi 
ambao walikuwa wakiendelea kumsaka.
“Msafara ulikuwa na 
magari mawili. Moja lilitumika kwa uangalizi, lingine lilimbeba Sheikh 
Ponda. Tulipofika Chalinze tulikuta kizuizi tukakikwepa kwa kupitia 
Msata kisha Bagamoyo hadi Dar es Salaam na kumfikisha Muhimbili,” 
alisema.
  
 
Msemaji
 wa familia ya Sheikh huyo, Isihaka Rashid alisema hawaitambui tume 
iliyoundwa na polisi kwa kuwa jeshi hilo ndilo linalotuhumiwa.
  
 
“Tunachofanya
 hivi sasa ni kukusanya ushahidi wetu, kwa bahati nzuri tayari tumepata 
mkanda wa tukio lenyewe ambao utatuwezesha kumbaini aliyemshambulia 
Sheikh Ponda.
 
“Hatuwezi kuhitaji majibu ya hiyo 
tume yao na hata leo kuna maofisa wa polisi kutoka Makao Makuu na Kituo 
cha Kati, Dar es Salaam walifika wakitaka kumhoji eti kuhusu uchochezi 
lakini alikataa kuzungumza hadi mwanasheria wake awepo, wakaondoka,” 
alisema Rashid.
Mwananchi
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment