Kyela. Imependekezwa kuwa Katiba Mpya itamke kuwepo kwa muundo 
wa Serikali moja ili kuweza kuulinda Muungano na kuondoa migogoro na 
migongano ya kimaslahi katika mgawanyo wa rasilimali.
                
              
Mapendekezo hayo yametolewa na Wajumbe wa Baraza 
la Katiba la Wilaya ya Kyela Mkoani Mbeya waliokuwa wakijadili ibara ya 
57 iliyohusu muundo wa muungano.
                
              
Diwani wa Kata ya Ngonga, Kileo Kamomenga alisema 
muundo wa Serikali mbili au tatu ni hatari, kwani unahatarisha Muungano 
na pia unatoa mwanya kwa Serikali moja kufanya uhusianona nchi nyingine 
ambazo hazitakuwa na nia njema na Watanzania .
                
              
“Kwa mfano katika ibara 62 kifungu kidogo cha (2) 
kinatoa uhuru kwa kila mshirika wa Muungano kuwa na uwezo wa kuanzisha 
uhusiano au ushirikiano na jumuiya au taasisi yoyote ya kikanda au 
kimataifa kitu ambacho mimi naona ni hatari kwa taifa letu, ni vema 
tukawa na Serikali moja, Zanzibar iwe ni moja ya mikoa ya Serikali moja 
ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,”alisema
                
              
Alisema kitendo cha Zanzibar kuwa na bendera yake,
 wimbo wake wa Taifa, Rais wake ni kuifanya kuwa nayo ni nchi 
inayojitegea na watu wake kujiita wao ni Wazanzibari na siyo Watanzania 
“Hivyo kama tuna lengo la kudumisha Muungano ni lazima tuwe na Serikali 
moja kuliko ilivyo hivi sasa,”alisema
                
              
Naye mjumbe, Clifford Mwaikinda alisema kuwa 
muundo wa Serikali moja utapunguza kubeba nzigo mkubwa kiuchumi na 
madaraka na kuwepo kwa usawa katika kugawanya rasilimali za nchi na 
kuondoa upendeleo kwa Serikali ya Zanzibar ambayo ilikuwa inanufaika na 
mambo mengi kutoka Tanganyika.
CHANZO:Mwananchi 
 
No comments:
Post a Comment