Maelfu wajitokeza kuandamana tena Misri
 
Maelfu ya wafuasi wa Rais wa Misri aliyeondolewa 
madarakani Mohammed Morsi wameanza maandamano mengine mjini Cairo, huku 
kukiwa na hofu ya kuzuka makabiliano zaidi. Maafisa wa usalama 
wamezingira barabara kuelekea medani ya Ramses ambapo maandamano hayo 
yalipangwa kufanyika. Maandamano ya sasa yanajiri siku mbili baada ya 
jeshi kuvunja kambi ambapo wafuasi wa vuguvugu la Muslim Brotherhood 
walikua wamesalia kwa zaidi ya mwezi mmoja.
                     
Makabiliano yalizuka na zaidi ya watu 600 
wakauawa, maelfu walijeruhiwa.Maandamano zaidi yanaendelea nje ya mji 
mkuu Cairo na taarifa zinasema watu wanne wameuawa kwenye makabiliano 
eneo la Ismailia. Polisi wa Misri wameamrishwa kutumia risasi za moto 
kulijinda na kulinda majengo ya serikali dhidi ya kushambuliwa.
                     
Huku utawala wa mpito ukitangaza hali ya 
hatari, mwandishi wa BBC aliyeko Cairo amesema taharuki imetanda mji 
mzima.Maelfu walikusanyika nje ya msikiti mmoja baada ya Muslim 
Brotherhood kuwaomba wafuasi wao kuandamana baada ya sala ya ijumaa 
wakiitaja kama siku ya hasira.
                     
                     
Magari ya kijeshi yanashika doria mjini Cairo, 
na njia ya kuingia medani ya Tahir kitovu cha maandamano ya mwaka 2011 
yaliyomuondoa madarakani Hosni Mubarak imefungwa. Huku haya yakiarifiwa 
wapinzani wa Mohammed Mosri pia wamepanga kuandamana dhidi ya mahasimu 
wao. Wakati huo huo watu wameombwa kulinda makaazi yao, makanisa na 
biashara. Wakristo nchini Misri wamekuwa wakilengwa katika siku za 
karibuni na makundi ya kiisilamu yenye misimamo mikali. Jumla ya 
makanisa 25, makaazi na biashara yalishambuliwa hapo Jumatano na 
Alhamisi.
chanzo;BBC 
 
 
 
          
      
 
  
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment