Vurugu Misri: Cairo kimya baada ya vifo.
 
Mji mkuu wa Misri Cairo umeripotiwa kuwa kimya, baada
 ya operesheni ya kinyama dhidi ya waandamanaji wanaomuunga mkono rais 
aliyepinduliwa Mohammed Morsi kupelekea vifo vya mamia ya raia. Mauaji 
hayo yamezua shutuma kutoka jamii ya kimataifa.
                     
                     
Zaidi ya watu 278 waliuwawa wakati maafisa wa 
usalama waliposhambulia kambi mbili za wafuasi wa Bwana Morsi. Kambi 
hizo zilianzishwa mwezi uliopita kupinga hatua ya jeshi kumng'oa rais 
huyo anayezingatia itikadi za kiislamu.
                     
Hali ya hatari imetangazwa na amri ya kutotoka nje nyakati za usiku kutolewa katika miji mikuu ya Misri.
                     
Waziri wa mashauri ya nchi za kigeni wa marekani
 John Kerry amesema matukio ''mabaya'' yaliyotokea ni ''pigo kubwa kwa 
juhudi za maridhiano''.
                     
Afisa wa mashauri ya kigeni katika Muungano wa 
Ulaya, EU, Catherine Ashton na katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban 
Ki-moon kadhalika wamekosoa hatua ya maafisa wa usalama kutumia nguvu 
dhidi ya raia.
                     
Raia wa Misri wanaamkia siku nyingine yenye 
shaka juu ya mustakabal wao, anasema mwandishi wa BBC Bethany Bell 
aliyepo mjini Cairo.
                     
Hata baada ya amri ya kutotoka nje kuondolewa 
Alhamisi asubuhi, kumekuwa na magari machache katika barabara za 
katikati mwa Cairo na madaraja yanayovuka mto Nile, anasema mwandishi 
wetu.
                     
'Pigo kubwa'
                     
Waandamanaji wamekuwa wakiitisha bwana Morsi aliyetimuliwa na jeshi tarehe 3 Julai, kurejeshwa madarakani.
                     
Vuguvugu la undugu wa Kiislamu, Muslim 
Brotherhood, ambalo lilifadhili maandamano ya hivi punde katika medani 
ya Nahda na pia karibu na muskiti wa Rabaa al-Adawiya, limesema kuwa 
idadi ya kweli ya watu waliouwawa siku ya Jumatano inazidi 2,000.
                     
Kwa mujibu wa serikali ya mpito inayoungwa mkono
 na jeshi, raia 235 waliuwawa kote nchini, pamoja na maafisa wa polisi 
43. Tarakimu hizi haziwezi kuthibitishwa kwa njia iliyo huru.
                     
Bwana Kerry amesema juhudi za maridhiano ya kisiasa nchini Misri zimepata "pigo kubwa".
                     
"Hii ni hatua muhimu kwa Wamisri wote," 
akaongeza bwana Kerry. " Mkondo wa vurugu utaelekea tu kwa msukosuko 
zaidi, mkasa wa kiuchumi na mateso."
                     
Afisi ya katibu mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban 
Ki-moon imesema kuwa ''anasikitika kwamba maafisa wa Misri waliamua 
kutumia mabavu wakati Wamisri wengi wanataka taifa lao kusonga mbele kwa
 amani katika mfumo utakaoongozwa na Wamisri wenyewe ili kuafikia 
maendeleo na demokrasia".
                     "Akilaani vikali" vurugu zilitokea Bi. Ashton 
amesema kuwa " ni juhudi za pamoja pekee kati ya Wamisri wote pamoja na 
jamii ya kimataifa ndizo zitakazorejesha taifa hilo katika demokrasia 
inayowashirikisha wote na kukabili changamoto zinazokabili Misri"
CHANZO:BBC 
 
 
 
          
      
 
  
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment