HAYA NDO MASHITAKA ALIYOSOMEWA SHEIKH PONDA AKIWA HOSPITALINI 
 
 
KATIBU wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, Sheikh Ponda 
Issa Ponda (54), amesomewa shtaka akiwa kitandani katika Kitengo cha 
Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Upasuaji wa Mishipa ya Fahamu (MOI).
  Katika shtaka hilo, Ponda anadaiwa kuwahamasisha wafuasi wake kufanya kosa.
  
  Mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, Hellen Riwa, Mwendesha 
Mashtaka wa Serikali, Tumaini Kweka, alidai kuwa uhamasishaji huo 
ulifanyika sehemu mbalimbali nchini kuanzia Juni 2 hadi Agosti 11 mwaka 
huu.
  
  Kweka alidai kuwa kosa hilo ni kinyume cha sheria ya makosa ya jinai kifungu 390 na 35 ya kanuni za adhabu.
  
  Kutokana na shtaka hilo, Hakimu Riwa aliahirisha kesi hadi Agosti 28 
na kutoa agizo Sheikh Ponda aendelee kuwa chini ya uangalizi wa vyombo 
vya dola wakati akiendelea na matibabu.
  
  Baada ya Hakimu Riwa kuahirisha kesi, wakili wa mshtakiwa Nasoro 
Jumaa, alilaumu utaratibu uliotumika na kusema kuwa mahakama imefanya 
kazi nje ya muda wa kawaida wa saa za kazi za kiserikali.
  
  Alisema mawasiliano ya awali ilikuwa askari na Tume ya Haki  Jinai ya 
Jeshi la Polisi kufika hospitalini hapo kwa ajili ya kufanya mahojiano 
na Sheikh Ponda.
  
  Aliongeza kuwa baada ya maofisa hao kufika hali ya Sheikh Ponda 
haikuruhusu  mahojiano kufanyika na ilipofika saa kumi jioni kila mmoja 
alitawanyika.
  Jumaa alisema kuwa wakiwa wanakaribia geti la kutokea Muhimbili, 
walipigiwa simu kuwa Sheikh Ponda anasomewa mashtaka, hatua aliyodai 
kuwa iliwashangaza.
  
  “Kama walikuwa na dhamira ya kumsomea mashtaka wangetuambia, kwa kuwa 
ni haki ya msingi kwa mtuhumiwa kuwa na mwanasheria wake kwa ajili ya 
kujua taratibu zilizotumika,” alisema.
  
  Alisisitiza kuwa baada ya kupata hati ya mashtaka wanajiandaa kupinga 
kosa hilo kwa kile alichoeleza kuwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu 
haina uwezo wa kusikiliza kosa la aina hiyo.
  
  Aliongeza kuwa kabla ya kufikiwa kwa hatua ya kumsomea shtaka Sheikh 
Ponda, walishaandika barua ya kutokuwa na imani na Tume ya Haki Jinai ya
 Jeshi la Polisi katika uchunguzi wao kwa kile alichoeleza kuwa ni 
watuhumiwa wa kwanza katika tukio la kujeruhiwa kwa mteja wake.
  Awali kabla ya kesi hiyo kusomwa maeneo mbalimbali ya Hospitali ya 
Muhimbili hususan jirani na jengo alilolazwa Sheikh Ponda, yalikuwa 
yamezingirwa na makachero wa polisi wakiwa na magari matano ya Kikosi 
cha Kutuliza Ghasia.
  Magari mawili yenye namba PT 2072 na PT 2061 yalikuwa jirani na mlango
 wa kuingilia katika kitengo cha mifupa huku askari wakiwazuia wananchi 
wasiende kumuona Ponda kwa kile walichoeleza kuwa kuna shughuli za 
kiserikali zinaendelea.
  
  Miongoni mwa watu waliozuiwa ni wakili maarufu nchini, Profesa Abdallah Safari.
-Tanzania daima 
 
 
 
          
      
 
  
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment