WAJINGA NDIO WALIWAO
Paliondokea
 mtu katika kisiwa cha Unguja, enzi za Seyid Majid Bin Said, naye akikaa
 mjini. Na mtu huyu alikuwa hana kazi maalum, kazi yake ilikuwa ni 
kuwafuata Waarabu wakubwa wakubwa, na kupata manufaa yake kwao. Na kazi 
zamani hizo ilikuwa watu kufunga bidhaa na kwenda bara kufanya biashara,
 na kulima vyakula na kuuza.
Na
 yeye alikuwa mtu mmoja asiyetaka kazi ya namna hii. Hata hatima 
akaonelea mji haumweki. Akatafuta kanzu yake njema akavaa, na kilemba 
chake cheupe, na msahafu wake kwapani, akashika njia kwenda pande za 
mashamba kutarazaki. Na kazi aliyoichagua ni kazi ya ualimu kusalisha 
watu. Lakini yeye hajui kusoma hata herufi moja. Alichagua kwenda shamba
 kwa Wahadimu kwa kuwa huko ndiko walikokuwa wajinga wasiojua kusoma, na
 hata dini ya Kiislamu ilikuwa haijaingia kwao bado.
Basi
 Mwalimu akawasili Unguja Ukuu. Wahaimu walipomwona mgeni wakamkaribisha
 sana. Hata waliposikia kuwa yeye ni mwalimu wakazidi kumkaribisha na 
kumheshimu. Na yeye mwenyewe ikawa mchana kutwa kufunua msahafu, 
kutazama tu, watu wanadhani anasoma! Akapewa nyumba bure na chakula 
kwao. Hatima akawaambia, Jengeni msikiti nikusalisheni. Wahadimu 
wakajenga msikiti. Hata wakati wa kusali ulipojiri mwadhini hapana, 
maana wale wenyeji hawajui.
Basi ikawa kazi ya mwenyewe Mwalimu kuadhini. Lakini naye vilevile hajui kitu. Akasimama akaadhini hivi:- Allah
 Akbar! Allah Akbar! Wajinga ndio waliwao, Wajinga ndio Waliwao. Allah 
Akbar ! Watu wakajaa msikitini. Huyu mwalimu kama nilivyosema hajui 
kusoma, si kukuambia kusalisha! Lakini watu wamekwisha kuwamo msikitini,
 ikawa hana hila ila kusalisha. Akaenda panapo Kibla, akasalisha hivi:- 
M, m, m,m ,m,m Wajinga ndio waliwao, Amin.
Ikawa
 kila akisema M,m,m ,m,m ,m ,m Wajinga ndio waliwao, Wajinga ndio 
Waliwao, Wahadimu huitikia Amin! Ikawa kila akiinama na kuinuka maneno 
ni hayo hayo. Na Wahadimu wakidhani asema Kiarabu, wakawa wamekazana tu,
 Amin! Zilipokwisha sala wakatoka nje. Wahadimu wakamsifu sana mwalimu 
wao jinsi anavyosalisha vizuri. Ikawa hivi hali ya mambo kwa siku nyingi
 kupita. Wakamfanyia mshahara mwema.
Siku
 moja akatoka Malimu wa kweli mjini anayejua kusoma na kusalisha ili 
kwenda kutembea shamba. Akafika Unguja Ukuu. Akapata habari kama mjini 
pana Mwalimu mmoja arifu sana, ndiye anayesalisha msikitini. Na huyu 
mwalimu mgeni asiende kumtazama, akangoja mpaka wakati w sala.
Wakati
 wa sala ulipojiri akamsikia mwadhini anaadhini. Lakini maneno yake 
yakamstusha sana. Allah akbar! Allah akbar! Wajinga ndio waliwao. Allah 
akbar! Yule mgeni asiseme neno, akaenda msikitini, akakuta watu wamejaa.
 Na mbele yao panapo kibla yuko mtu anayemjua tangu mjini, naye kumjua 
kwake hajui kitu. Basi akamsogelea kule kule mbele ili amsikilize vema. 
Na mwalimu alipomwona huyu mgeni akastuka sana maana naye amjua tangu 
mjini. Akawaza kuwa leo uongo wangu utabainika. Lakini mara akili 
zikamjia hivi:- M,m,m,m,m Mwalimu usinibaini, nikipata sita, tatu zangu,
 tatu zako, Wajinga ndio waliwao Amin! Na maneno haya wakisikiana wao 
wawili tu, maana walikaaa karibu karibu. Akashika kusalisha kwa maneno 
yale yale. M, m,m,m,m,m Mwalimu usinibaini, Wajinga ndio waliwao, 
nikipata nane, nne zangu na nne zako, Amin. 
Akasalisha
 hivi mpaka mwisho, wakatoka. Walipotoka nje wale walimu wakaamkiana kwa
 vicheko sana. Watu walipowaona wanacheka,wakidhani wanacheka yao ya 
huku nje, maana wanajuana. Kumbe wanacheka yaleyale ya Msikitini: 
Mwalimu usinibaini, wajinga ndio waliwao, nikipata nane, nne zangu, nne 
zako. Wakakaa katika hali hii wakiwala wajinga, mpaka walipochoka, 
wakaja zao mjini na wingi wa mapesa.
Hadithi
 hii inatufundisha nini? na hali ya Tanzania tukiangalia hali halisi ya 
uwekezaji feki pamoja na mambo mengine. JE sisi pia sio miongoni mwa hao
 wajinga ndio waliawao?
 
 
 
          
      
 
  
 
 
 
 
 
 
 
 
 
 
No comments:
Post a Comment