Friday 19 July 2013

KONGONI OBAMA



1.      Karibu Obama kwetu, kwenye adhimu amani,

Twaona fahari kwetu, kukukirimu nyumbani,

Kifika ardhi ya kwetu, futashaka mtimani,

Tafrani hazipo kwetu, elewa hilo mwandani,

Kongoni Obama kwetu, Tanzania kwenye utu.



2.      Lako jio twastahi, sawa na mboni jichoni,

Sini tukutanabahi, ngefanya ziara nchini,

Asilati ubaguhi, licha ya sisi maskini,

Ni kama ndoto wallahi, santé kwa kututhamini,

Kongoni Obama kwetu, Tanzania kwenye utu.



3.      Sisi tunatamaduni , nzuri zenye kuvutia,

Tamaduni zimesheheni, tabia zake maridhia,

Zimesheheni tumaini, linalo tusaidia,

Tumaini li pomoni, na sisi twalitumia,

Kongoni Obama kwetu, Tanzania kwenye utu.



4.      Ziara takayo fanywa, nchini kwetu pande zote,

Ombi isije kuminywa, na kutufanya tupwite,

Hatutaki kukanganywa, nasi faida tupate,

Vile tulivyopokonywa, vilitufanya tujute,

Kongoni Obama kwetu, Tanzania kwenye utu.



5.      Mazungumzo yalenge, kututoa hawindeni,

Wanauchumi wapange, kutuweka kileleni,

Yalo kinyume tupinge, kama Malaria nchini,

Watu mikono tuunge, ziara yenye thamani,

Kongoni Obama kwetu, Tanzania kwenye utu.



6.      Hima iwe kichocheo, kwa rasilimali zetu,

Viwanda kama vya nguo, matunda vifufuliwe,

Uwekezaji wa kileo, tuupigie upatu,

Tutapata mandeleo, na uchumi uchanuwe,

Kongoni Obama kwetu, Tanzania kwenye utu.



7.  Nia kama tukiweka, kukacha wetu uvivu,
Mikataba kuanika, itauzika uovu,
Kiongozi chakarika, ziada ni ushupavu,
Marudi nayaandika, kuepuka maumivu,
Kongoni Obama kwetu, Tanzania kwenye utu.

8.      Jama Barack  Obama, karibia Tanzania,
Ziara fanya salama, Kikwete  atarajia,
Jio litazaa chema, kwa taifa zetu pia,
Urudipo rudi vyema, huku si twakuombea,
Kongoni Obama kwetu, Tanzania kwenye utu.


No comments:

Post a Comment