JESHI
 la Polisi mkoani Katavi limemtia nguvuni Masaga Charles (36) akidaiwa 
kuwa muuaji wa kukodiwa. Charles ambaye pia alikuwa bingwa wa mashindano
 ya mbio za baiskeli yaliyofanyika Arusha mwaka jana, anatuhumiwa 
kufanya mauaji ya ukatili wilayani Mpanda. 
Inaelezwa kuwa kwa zaidi ya miaka 15, Charles amekuwa akishiriki katika 
mashindano ya mbio za baiskeli katika mikoa ya Tabora, Shinyanga, Mwanza
 na Arusha Oktoba mwaka jana ambako aliibuka mshindi na kujinyakulia Sh 
800,000.
Kwa mujibu wa Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Katavi , Dhahiri Kidavashari,
 mtuhumiwa huyo ni mkazi wa Kijiji cha Chilalo Wilaya ya Misungwi mkoani
 Mwanza.
Charles anatuhumiwa kumuua Moshi Bella (44) wa Kijiji cha Karema kwa 
kumkatakata na panga kichwani na shingoni baada ya kuahidiwa kulipwa Sh 
milioni tano.
Kamanda Kidavashari alisema tukio hilo la mauaji ya kinyama lilitokea 
Julai 21 mwaka huu katika Kijiji cha Kabange Kata ya Simbwesa Tarafa ya 
Kabungu mkoani Katavi.
Alisema mtuhumiwa kabla ya kufanya mauaji hayo alionana na Bella akijifanya alikuwa anataka auziwe shamba.
Mazungumzo hayo yalifanyika Julai 20 mwaka huu nyumbani kwa Salumu 
Kajimba ambaye ni ndugu wa marehemu Bella, alisema Kamanda Kidavashari.
Kamanda alisema mtuhumiwa na Bella walikubaliana kuuziana ekari mbili za shamba ambalo ni mbuga ya mpunga.
“Walikubaliana kuuziana Sh 300,000 kwa kila ekari na baada ya 
makubaliano hayo mtuhumiwa alimuahidi Bella kwamba angerejea siku ya 
pili kwa ajili ya kutoa malipo hayo,” alisema Kamanda.
Alisema siku iliyofuata mtuhumiwa Charles alifika nyumbani kwa Salumu 
Kajimba ambaye ni ndugu wa Bella ya saa 9.00 alasiri lakini bahati mbaya
 Bella alikuwa amekwenda kisimani kuoga.
Mtuhumiwa baada ya kuambiwa Bella alikuwa amekwenda kisimani alimuaga Kajimba na mkewe akisema alikuwa anamfuata Bella.
Kamanda Kidavashari alisema Bella hakuonekana nyumbani tangu alivyowaaga
 kuwa anakwenda kuoga kisimani wala Bella aliyemfuata naye hakurejea 
hadi hapo mwili wa Bella ulipookotwa mbugani.
Mwili wa Bella ulikutwa umekatwakatwa na panga shingoni kwa nyuma na kichwani.
Kamanda alisema baada ya polisi kuarifiwa na raia wema kuhusu mauaji 
hayo waliweza kumkamata mtuhumiwa Masaga Charles katika mtaa wa 
Makanyagio mjini Mpanda.
Baada ya kukamatwa mtuhumiwa alikiri kuhusika na mauaji hayo akidai 
alitumwa na mkazi mmoja wa Kijiji cha Iroba Tarafa ya Kabungu wilayani 
Mpanda aliyemuahidi kumlipa Sh milioni tano.
Kamanda
 alisema mtuhumiwa alidai kuwa mtu aliyemtuma amekwisha kukimbilia 
mkoani Shinyanga ili asijulikane kuwa ndiye aliyehusika na mpango wa 
mauaji hayo.
Mtuhumiwa alidai kuwa kwa mara ya kwanza aliambiwa kufanya mauaji hayo 
Oktoba mwaka jana kwa malipo ya Sh milioni mbili lakini alikataa, 
alisema. Kamanda alisema mtuhimiwa alidai kuwa Aprili mwaka huu 
aliambiwa tena afanye mauaji kwa malipo hayo lakini akaendelea kukataa 
hadi alipoongezewa dau na kufika Sh milioni tano na kupewa shamba la 
ekari mbili.
Mtuhumiwa anatarajiwa kufikishwa mahakamani wakati wowote kujibu tuhuma za mauaji zinazomkabili, alisema kamanda.
source: Gazeti  la  mtanzania
 
No comments:
Post a Comment