Thursday 26 March 2015

Prof. Baregu: Zitto ni mzigo

Profesa Mwesiga Baregu
         PROFESA Mwesiga Baregu

PROFESA Mwesiga Baregu, mmoja wa watu wanaoheshimika nchini amesema, aliyepata kuwa Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe, anaponzwa na kibuli cha kujiona hakuna zaidi ya yeye.

Amesema, Zitto ambaye alikuwa naibu katibu mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tanzania Bara na naibu kiongozi wa upinzani bungeni, anafanya kazi asiyoifahamu na ambayo haina mavuno.


“Ninamfahamu vizuri. Wakati tuhuma hizi za usaliti zilipoanza kuibuka, Kamati Kuu ilinikabidhi jukumu la kumsaidia mama yake mzazi kumlea kijana huyu.”

Kauli ya Baregu ilitolewa siku moja baada ya Zitto kujiondoa bungeni na baadaye kujiunga na Chama cha ACT – Tanzania.

Prof. Baregu aliwahi kuwa “mlezi wa Zitto” ndani ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema). Alikabidhiwa jukumu hilo na Shida Salum, mama mzazi wa Zitto (marehemu), baada ya mama huyo kuiomba Kamati Kuu (CC) ya chama hicho “kusaidia kumlea.”

Prof. Baregu ambaye ni mjumbe wa kamati kuu ya Chadema anasema, “Zitto hamnazo. Amekuwa anajiona yeye ni zaidi ya chama. Hashauriki.”

Anasema wakati ule alipopewa kazi ya kumlea Zitto “katikakati ya migogoro, tulikuwa tunazungumza naye mara kwa mara. Ninamfahamu. Kazi hii ya kumlea tulikabidhiwa mimi na mama yake mzazi, Bi. Shida Salum,” anaeleza Baregu.

Mama mzazi wa Zitto, alifariki dunia Juni mwaka jana, baada ya kuugua kwa muda mrefu.
Kauli ya Prof. Baregu ilifuatia gazeti hili kutaka maoni yake juu ya mustakabali wa kisiasa wa Zitto baada ya kuwahi kujiondoa ndani ya Chadema.

No comments:

Post a Comment