1.0.         Libya ni moja kati ya nchi wafadhili
 wa Tanzania ambapo, kama ilivyo wafadhili wengineimekuwa ikiipa nchi 
yetu misaada na mikopo yenye masharti nafuu. Serikali yetu imekuwa 
ikifanya taratibu mbalimbali kulipa madeni ya nchi wafadhili kwa njia 
mbalimbali ikiwa ni pamoja na utaratibu wa kubadili madeni na kuyaingiza
 katika miradi n.k, yaani ‘Dept Swap’.
 2.0.         Katika utaratibu huo wa ‘Dept Swap’, tarehe 20/7/2005, 
Serikali ya Tanzania na Libya zilitia sahihi mkataba wa Dept Swap (Dept 
Swap Agreement) ambao uliweka utaratibu wa matumizi na urejeshaji wa 
fedha za deni la Libya.
 3.0.         Tarehe 4/3/2009, Serikali ya Libya na Tanzania zilitia 
sahihi mkataba wa nyongeza (Addendum to the Dept Swap Agreement) ambao 
ulizungumzia, pamoja na mambo mengine, matumizi ya jumla ya dola za 
Kimarekani milioni 20 (20,000,000) ambazo zilikuwa zimehifadhiwa katika 
akaunti ya Libya No.004-200-0002216-01, Benki ya Rasilimali Tanzania 
(Tanzania Investment Bank).
 4.0.         Nyongeza hii ya mkataba ilitamka bayana katika kifungu 
No.4.02, kwamba, fedha zilizokuwa katika akaunti tajwa, zikopeshwe kwa 
mwekezaji waliyemteua wao wenyewe, ambaye ni kampuni ya MEIS INDUSTRIES 
LIMITED kwa ajili ya mradi wa ujenzi wa kiwanda cha Saruji Lindi. Kwa 
mujibu wa nyongeza hii, mkopo ulipaswa kulipwa ndani ya miaka sita, na 
baada ya hapo, fedha hizo zirejeshwe na ziendelee kukopeshwa Watanzania 
kwa ajili ya miradi mingine ambayo Serikali za Libya na Tanzania 
zitakuwa zimeridhia.
5.0.         Kumbukumbu zinaonyesha mambo mawili:-
5.1 Kwamba, kabla ya Serikali ya Libya kutia sahihi nyongeza hii ya 
mkataba iliyotaka fedha zikopeshwe kwa MEIS INDUSTRIES, upembuzi 
yakinifu wa mradi husika ulifanywa na serikali ya Libya kupitia vyombo 
vyake, na wao wenyewe walishajiridhisha juu ya ubora wa mradi huo 
(Viability of the Project)
 5.2 Kwamba, baada ya kutia sahihi nyongeza ya mkataba, Serikali ya 
Libya kupitia Ubalozi wake hapa nchini iliendelea kusisitiza kwa 
maandishi kwamba Serikali ya Tanzania iharakishe mchakato wa kuwezesha 
fedha hizo zikopeshwe kwa mwekezaji waliyemteua ili mradi huo muhimu 
usiendelee kuchelewa, na pia fedha ziingie katika mzunguko kwa manufaa 
ya Watanzania.
6.0. Katika kutekeleza mikataba hii miiwli, yaani Dept Swap Agreement ya
 tarehe 20/7/2005 na Addendum Dept Swap Agreement ya Tarehe 4/3/2009, na
 kwa kuzingatia umuhimu ambao serikali ya Libya iliuonyesha, Serikali ya
 Tanzania kupitia watalaamu wake wa Wizara ya Fedha, Benki ya Rasilimali
 (TIB) na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, na Mwekezaji (Kampuni ya MEIS), 
walikutana chini ya usimamizi wa Wizara ya Fedha na kuandaa hadidu za 
rejea ambazo zilipelekea kutengenezwa kwa mkataba wa uwekezaji 
(Investment Agreement) kati ya serikali ya Tanzania, TIB, Serikali ya 
Libya na Mwekezaji.
 7.0. Serikali ya Tanzania, TIB na Mwekezaji walitia sahihi mkataba huu 
na kuupeleka Libya ili serikali ya Libya ipate kuweka sahihi. Kwa sababu
 ambazo hazikufahamika, serikali ya Libya haikutia sahihi mkataba huo.
 8.0. Baada ya kufuatilia kwa muda mrefu bila mafanikio, mwekezaji 
alimuandikia barua Mwanasheria Mkuu wa Serikali ya Tanzania yenye 
kumbukumbu No. PC/MEIS/AG/2/10 ya tarehe 1/9/2010 akieleza kusudio la 
kuipeleka Serikali ya Libya Mahakamani kwa kitendo chake cha kutokutia 
sahihi mkataba.
 9.0. Terehe 13/9/2010, Mwekezaji alifungua shauri Mahakama Kuu ya 
Tanzania, shauri la madai No. 124/2010 dhidi ya serikali ya Libya, 
akiiomba Mahakama Kuu itoe tamko kwamba kitendo cha serikali ya Libya 
kukataa kutia sahihi mkataba huu hakikuwa kitendo cha haki na kwamba 
mahakama itoe amri kwamba fedha hizo zitolewe kwa Mwekezaji ili 
kutekeleza mradi uliokusudiwa.
Kumbukumbu zinaonyesha kwamba wito wa Mahakama (Summons) ulipelekwa 
Ubalozi wa Libya lakini hapakuwa na majibu wala mwakilishi aliyekuja 
mahakamani.
10.0. Mahakama Kuu, kwa kufuata taratibu zake, iliendelea na kusikiliza 
shauri na kutoa amri kama ambavyo mahakama yenyewe ilijiridhisha. Amri 
ya mahakama, pamoja na mambo mengine, iliagiza kwamba fedha hizo 
zitolewe kwa mwekezaji ili kutekeleza mradi husika.
 11.0. Zilifanyika juhudi za Benki ya Rasilimali (TIB) pamoja na Ofisi 
ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kupinga au kupata ufafanuzi zaidi juu ya
 amri hiyo ya utekelezaji wake. Mahakama Kuu pamoja na Mahakama ya 
Rufana, katika nyakati tofauti, zilishughulikia maombi hayo na 
kuyafikisha katika hatima yake kwa mujibu wa sheria. Kwa ajili ya 
kumbukumbu, mashauri yaliyofunguliwa ni kama ifuatavyo:-
   11.1 TIB ilifungua maombi No. 126/2010 katika mahakama ya Rufaa 
kuiomba izuie na kufuta utekelezaji wa amri ya Mahakama Kuu. Maombi haya
 ya TIB yalifanyiwa uamuzi wa mwisho mnamo tarehe 7/11/2011, ambapo 
maombi hayo yaliondolewa mahakamani kwa kuwa, kwa mujibu wa Mahakama ya 
Rufaa, hayakuwa yamefuata taratibu za kisheria.
  11.2 Mwanasheria Mkuu wa Serikali naye akapeleka maombi Mahakama ya 
Rufaa. Maombi ya kwanza, maombi namba .146/2010 akiomba Mahakama ya 
Rufaa kufuta mwenendo mzima wa kesi pamoja na amri ya Mahakama Kuu, na 
maombi ya pili No. 147/2010 ikiiomba Mahakama ya Rufaa izuie utekelezaji
 wa amri ya mahakama Kuu (Stay of Execution). Maombi haya yote 
yalisikilizwa na kuamuliwa kwa mujibu wa sheria na taratibu za 
kimahakama.
 12.0 Wakati haya yakiendelea, ilijitokeza kampuni ya Mohamed 
Enterprises Limited ikidai kwamba ina haki juu ya fedha hizi. Nayo 
ikafanya yafuatayo:-
    12.1 Ilipelea maombi Mahakama Kuu kuzuia utekelezaji wa hukumu kwa 
madai kuwa kampuni hiyo  nayo ilikuwa ikiishtaki Serikali ya Libya 
katika kesi ya madai No. 110/2010 na kwa hiyo, endapo amri ya Mahakama 
Kuu ingetekelezwa kwa kumpa mwekezaji (Kampuni ya MEIS) fedha za Libya, 
basi wao (Mohamed Enterprises Limited) wangekosa mahali pa 
kutekeleza/kukazia hukumu waliyokuwa wakiitarajia katika kesi yao (no. 
110/2010) dhidi ya serikali ya Libya. Maombi haya yalisikilizwa na 
Mahakama Kuu na kutolewa maamuzi stahiki.
       12.2. Kampuni ya Mohamed Enterprises Limited haikuridhika na 
uamuzi wa Mahakama Kuu kwa hiyo kapeleka shauri hili Mahakama ya Rufaa, 
kupitia maombi (Civil Revision) No. 2/2011. Maombi haya nayo pia 
yalisikilizwa na kutolewa maamuzi.
 13 Mwisho wa yote maamuzi ya Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa katika 
mchakato mzima yakawa kwamba mwekezaji (Kampuni ya MEIS) alikuwa na haki
 ya kupewa fedha za mradi wa Kiwanda cha Saruji Lindi kama ilivyoanishwa
 katika mkataba kati ya serikali ya Tanzania na Libya. Ni dhahiri 
kwamba, mgogoro huu ulichujwa na mahakama mpaka ngazi ya juu kabisa, 
tena kwa nyakati tofauti na mbele ya waheshimiwa majaji wa Mahakama Kuu 
na Mahakama ya Rufaa.
14.0 Katika Taifa linaloongozwa kikatiba, chini ya utawala wa sheria 
kama Tanzania, ambapo Mahakama ndicho chombo kilichopewa mamlaka ya 
mwisho kuamua juu ya haki za raia na hata serikali, si rahisi na wala 
haitakuwa sahihi kwa mtu yeyote kuhoji uhalali wa mchakato huu kama 
ulivyoongozwa, kuelekezwa na kuamuliwa na mahakama, isipokuwa tu kama 
sheria inatoa mwanya mwingine kurudi mahakamani kwa mtu yeyote ambaye 
hajaridhika au anayetaka kuhoji maamuzi haya kwa namna yoyote.
 15. Mahakama iliamua kwa mujibu wa sheria. Na kwa kuwa hakuna 
aliyeendelea kupinga kimahakama, suala hili lichukuliwe kwamba limefikia
 mwisho na limefungwa. Lakini hata kiuongozi, na hasa kwa mtu yeyote 
mwenye kutazama maslahi ya Taifa hili, ni dhahiri kwamba suala la 
utekelezaji wa mikataba ya kubadilishana madeni ni jambo lenye manufaa 
kwa Tanzania na linapaswa kila fursa inapojitokeza kutekelezwa haraka. 
Wenzetu, nchi wafadhili, wanapotoa fursa za kutupunguzia mzigo wa madeni
 katika utaratibu wenye manufaa kama huu, tutaendelea kuonekana wa ajabu
 kama tutaendelea kulumbana badala ya kuchangamkia fursa ya maendeleo. 
Tukwepe mazingira yanayopelekea taifa letu kuonekana kama wale watoto 
watukutu waliokabidhiwa zawadi ya nyumba, badala ya kuishi kwa shukrani 
ya nyumba ile, wakagombana na kunyang’anyana fito na kuzitumia kupigana 
bila kujali kwamba nyumba inaanguka maana fito ndizo zilizo ishikilia.
 16.0 Mimi kama Mbunge kutokea Mkoa wa Lindi, na kama Waziri mwenye 
dhamana ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, nalifuatilia kwa 
karibu suala hili kwa sababu mbili:-
 (i) Kwanza, kuanzishwa kwa mradi huu kutawanufaisha wapiga kura wangu, 
na Watanzania kwa ujumla kwa kuinua uchumi wetu na kuongeza ajira hasa 
wa Mikoa ya Kusini ambayo imeachwa nyuma kwa muda mrefu. Utafiti 
unaonyesha kuwa Mikoa ya Lindi na Mtwara ina utajiri mkubwa wa mali 
ghafi ya Saruji, na kwa hiyo upo uhakika wa kupata saruji bora na kwa 
bei nafuu sana.
 (ii)  Pili, suala hili linagusa mahusiano ya Nchi mbili kwa hiyo lazima
 Wizara yangu ilisimamie kwa nguvu, umahiri na umakini wote.
 17.0 Kama nilivyosema huko nyuma, fedha zote zilizotolewa kwa amri ya 
Mahakama ni Mkopo. Hazikuchukuliwa kama fedha za EPA au ESCROW. Ni mkopo
 uliotolewa kwa Kampuni ya MEIS kwa mujibu wa Mkataba wa Makubaliano 
(Investment Agreement) yenye Masharti Kibenki. Na Masharti hayo ya 
Kibenki yanamtaka Mwekezaji kuweka dhamana, kulipia riba, kuwekewa muda 
wa kurudisha mkopo, na anawekewa hatua za kuchukuliwa endapo Mwekezaji 
huyo atashindwa kulipa mkopo. Kwa lugha nyingine, Kampuni ya MEIS 
ikishindwa kulipa mkopo huo, itafilisiwa mali zake na TIB itarudishiwa 
fedha zake. Iacheni benki ifanye kazi yake. Mkopo unageukaje kuwa 
ufisadi?
 18.0 Mimi sina Kampuni hapa nchini. Sina ubia na kampuni yoyote ikiwemo
 Kampuni ya MEIS. Sina hisa katika Kampuni ya MEIS. Na sijafaidika na 
mkopo huo ambao unasimamiwa na Benki ya Uwekezaji nchini (TIB). Ndiyo 
maana uvumi kuwa nahusika na ufisadi wa mabilioni ya Libya hauna mashiko
 kabisa. Baadhi ya wanasiasa wenzangu wanajua ukweli wote huu lakini kwa
 makusudi wanaamua kuwafanya watu waamini wapinzani!
 19.0  Ujenzi wa kiwanda cha simenti cha Lindi unaendelea vizuri na  
mitambo yote inayotakiwa katika ujenzi huo imekwisha wasili. Asilimia 45
 ya ujenzi wa kiwanda hicho umekamilika na ni mategemeo ya kampuni ya 
MEIS kuwa kiwanda hicho kitakamilika ifikapo mwezi Disemba mwaka huu wa 
2015.
 20.0  Ni matumaini yangu kuwa nimeeleweka vya kutosha. Kama kuna mtu 
anahitaji taarifa zaidi basi awe huru kuihoji kampuni ya MEIS na Benki 
ya TIB ambayo imetoa mkopo huo, au kumpata Msajili wa Mahakama Kuu na 
Mahakama ya Rufaa ambazo zote ziliamua Kampuni ya MEIS ipewe mkopo huo 
kwa mujibu wa sheria za kibenki.
 Bernard K. Membe (Mb)
 WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA
 USHIRIKIANO WA KIMATAIFA
 
No comments:
Post a Comment